Monday, November 24, 2008

'MIAKA 30 KWA WANAOWAPA MIMBA WANAFUNZI'

Kitendo cha kumpa mimba mwanafunzi (wa chekechea hadi sekondari) au mtoto yeyote aliye na umri chini ya miaka 18 si tu kinamharibia mtoto husika muelekeo wake wa kimasomo/ kimaisha kwa baadae,hasa anapolazimika kuigawa akili yake darasani na katika kumlea mtoto, bali pia ni ukatili wa hali ya juu dhidi ya haki za mtoto wa kike.Kitendo hiki kinafaa kulaaniwa na walimwengu wote wanaothamini na kuwaheshimu watoto.

Hivi karibuni Serikali imekuwa mbogo katika kutekeleza mikakati mbalimbali kuhakikisha watoto wa kike wanalindwa dhidi ya mimba za utotoni ikiwa ni pamoja na kupitishwa kwa sheria inayotoa kifungo cha miaka 30 kwa anayempa mimba au kufanya mapenzi na mwanafunzi. Jitihada hizi zinafaa kupongezwa na kila Mtanzania hasa mzazi. Utokomezaji wa vitendo hivyo hautafanikiwa iwapo jamii itaiachia serikali peke yake ilishughulikie swala hili kwani kufanikiwa kwake kikamilifu kutatokana na jamii kuepukana na mfumo dume unaoangalia mwanamke kama chombo cha starehe au chanzo cha mapato kisichokuwa na maamuzi yoyote. Jamii ikilielewa hili itaacha kuwaozesha watoto wa kike mapema mara tu wanapopevuka na pia itaacha mazoea ya kwenda kujadiliana mambo ya mahari baada ya mtoto kupewa ujauzito au kufumbia macho vitendo hivi vinapotokea na badala yake itaanza kufikilia namna gani mtoto huyu aliyekatiliwa aweze kufarijiwa na kumjengea msingi wa maisha yake ya baadae ikizingatiwa kuwa kuteleza sio kuanguka.

Lazima tukubaliane kwanza kuwa mimba hizi za utotoni wasababishaji ni watu wazima, wengine wakiwa na familia zao pamoja na utukutu au malezi mabovu ya baadhi ya watoto na hivyo kujikuta wakipeana mimba wao kwa wao iwe kwa makubaliano au kwa kubakwa.Kwa msingi huu ni dhahiri kuwa hata adhabu zitakazotolewa kwa wahusika lazima zitatofautiane.

Maswala la kujadili:

  • Iwapo mwanaume aliyempa binti/mwanafunzi mimba amefungwa nani atawajibika kutoa gharama za malezi ya mtoto baada ya kuzaliwa?

  • Kitendo cha kuumfunga mwanaume aliyempa mimba mwanafunzi miaka 30 sio chanzo kingine cha kuzalisha chokoraa mitaani kutokana na uwezekano wa watoto hawa kukosa malezi ya wazazi wawili?

  • Mtoto anapoambiwa / anapogundua kuwa kuna mtu (baba yake) yupo gerezani kwa kosa la kusababisha yeye azaliwe kisaikolojia mtoto anakuwa katika hali gani?aaatawatafsiri vipi watu atakaogundua kuwa hawakufurahishwa na kuzaliwa kwake hadi wakamfunga aliyesababisha kuzaliwa huko?

Kutokana na maswala hayo yanayojitokeza hapo juu, je kuna haja ya kuamua kwamba wanaowapa mimba wanafunzi/watoto:

  • Wahasiwe ili wasiendeleze tabia hiyo tena na wasifungwe ili wabaki wanahudumia watoto wao
  • Baadhi ya mali zao zichukuliwe na mtoto aliyepewa ujaozito kwa ajili ya malezi ya mtoto atakayezaliwa
  • Walazimishwe kuwasomesha wanafunzi waliowampa mimba baada ya kuzaa
  • Familia za wanaume wanaowapa mimba wanafunzi zichukue jukumu la kuwalea na kuwasomesha wanafunzi wakishajifungua wakati waliowapa mimba wakiwa wanatumikia vifungo.
  • Walazimishwe kumtunza mtoto wa kike pamoja na mtoto, kwa mtoto malezi yawe hadi atakapoanza kujitegemea na kwa mwanamke iwe hadi atakapoolewa au vinginevyo

Naomba tushirikiane kulijadiliiswala hili ili kutoa msaada endelevu katika maisha ya mtoto wa kike baada ya kujifungua. je adhabu inayotolewa inamsaidia vipi mtoto wa kike aliyekwishapatwa na dhahama hilo?

No comments: